Tuesday 23 February 2021

NAMNA SIMU YAKO INAVYOATHIRI MFUMO WA USINGIZI

 Uchunguzi uliofanywa na Tume ya Usingizi ya Marekani mwaka 2011 uliokuwa na kichwa cha, “Mawasiliano ndani ya chumba cha kulala,” uligundua kwamba asilimia 95 ya walishiriki walitazama simu zao  ndani ya saa moja kabla ya kwenda kulala.

 

Mwaka 2016 uchunguzi ulifanywa kwa vijana 2750 huko Uingereza uligundua kwamba 45 asilimia walisema kwamba wamekuwa wakicheki simu zao wakiwa usingizini na 42 asilimia walisema walilala na simu karibu kabisa na kitanda chao.

                           

Pia, uchunguzi uliofanywa na kampuni ya Accel na Kampuni ya Teknolojia ya data Qualitrics, unasema kwamba asilimia 53 ya vijana wa kizazi kipya hutazama barua pepe zao(emails) katikati ya usiku wa manane.

Naye mwandishi Catherine Prince anasema, asilimia 80 ya Waamerika hutazama  simu zao katika kipindi cha nusu saa toka wanapokuwa wameamka.

                             

Takwimu zinasema kwamba nusu yetu hutazama simu zetu usiku wa manane tukishtuka toka usingizini (Vijana wenye miaka 25-34 ni zaidi ya 75 asilimia)

Inawezekana takwimu zote nilizozitaja hapo juu zinakuhusu kwa namna moja ama nyingine. Ni wachache wetu hawana tabia ya kuweka simu mbali na kitanda wanacholalia, tena wengine huweka simu zao chini ya mito wanayolalia. 

                                              

Ni wazi pia kwamba, watu wengi hutazama simu zao mara tu waamkapo. Yaani wengi wa watu siku hizi kitu cha kwanza wanachokumbuka mara tu waamkapo ni simu zao.

Je simu zetu zinaathiri vipi mifumo yetu ya usingizi?

Kila usiku saa mbili hadi tatu kabla ya muda wako wa kulala, kuna kitu homoni ambayo huzalishwa kwenye ubongo wako, homoni hiyo huitwa kwa kitaalamu melatonin. Melatonin  huuambia mwili wako kwamba sasa ni usiku hivyo unapaswa kusinzia.

Kukikucha ambapo mwanga wake ni wa bluu, mwanga huu hupiga nyuma ya jicho asubuhi, na ubongo wako huacha kutoa melatonin.Unajisikia kuamka na tayari mwili wako upo tayari kuianza siku.

Muda unapofika na mwanga wa bluu ukaanza kupotea (pale linapokuja giza au taa za umeme zinapowashwa), melatonin huanza kutoka tena.

Unajua ni kitu gani kingine hutoa mwanga wa bluu? Simu. Pale tunapotumia simu zetu, au kopyuta mpakato kabla ya kwenda kulala, mwanga wa bluu huwa unauambia ubongo wako kwamba sasa ni mchana lazima huwe macho. Kwa namna nyingine tunaifanya mifumo yetu ya mwili iende tofauti na vile tunavyopaswa kuwa na kuharibu mfumo wa ubora wa usingizi tunaopaswa kulala.

 Kushika simu zetu mara tu kabla ya kulala ndicho kitu kinatufanya muda mwingine tushtuke usiku wa manane na kushika simu tukiangalia yale yaliyojili wakati tumelala. Wengine wamekua wakikosa usingizi kiasi kwamba hata muda wa kufanya kazi wanasinzia. Hawa ni watu wanaoua usiku.

Kutokana na kitengo cha Afya ya Usingizi cha Chuo Kikuu cha Harvard cha nchini Marekani wanasema, kuwa na usingizi wa muda mfupi “Inaweza kuathiri uwezo wa kuhukumu, unavyojisikia (mood), uwezo wa kujifunza na uwezo wa kutunza kumbukumbu na inaweza kuleta athari mbaya za ajari na majereha.”

Baadhi ya waliofanya chunguzi kuhusu usingizi wamepata matokeo kwamba kupungua kwa muda wa usingizi unaweza kusababisha unene wa kupindukia na magonjwa ya siku hizi kwasababu ya kupungua kwa mfumo wa mmeng’enyo wa chakula unaotokana na muda wa kupumzika.

Hata matumizi kidogo yam wanga yanaweza kusababisha upungufu wa usingizi. Uchunguzi uliofanywa na wachunguzi wa Chuo Kikuu cha Harvard uligundua kwamba ukitumia IPad kusoma usiku kabla ya kwenda kulala inasababisha kutozalishwa kwa kemikali ya melatonin kwa asilimia 53.

Kupitia chunguzi hivyo ni vyema mno kupunguza ukaribu na simu zetu nyakati za usiku. Kuna vitu vingi sana ambavyo tumekuwa tukivifanya kwenye simu zetu kama mazoea na hatujui kama vina athari kubwa kwetu.

Mambo ya kufanya;

Punguza matumizi ya simu nyakati za usiku.

Hakikisha haulali karibu na simu yako, iweke mbali hii itakusaidia kuepuke tabia ya kushika simu yako usiku wa manane.

Iweke simu yako katika ukimya (silence) ili unapoingia ujumbe wowote wakati wa usiku usikulazimishe kushika simu yako.

Imeandaliwa na

Edius Katamugora

0764145476

ekatamugora@gmail.com 

Hii ni blogu rasmi ya Edius Katamugora, hapa utajifunza maendeleo binafsi, utapata makala mbalimbali zinazohusu biashara, elimu, hamasa na maisha kwa ujumla. Karibu sana katika blogu hii.

0 comments: